RAIS WA SINGAPORE AWASILI NCHINI,KWA ZIARA YA KITAIFA YA SIKU 3 NCHINI
Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam akiwa ameambatana na Mwenza wake Mama Jane Ittogi, alilakiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mahmoud Thabit Kombo(Mb) ambaye aliambatana na viongozi wengine waandamizi wa serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania, Mhandisi Peter Ulanga.
Ziara ya Kitaifa ya Rais Tharman Shanmugaratnam, ni ya kwanza kufanywa na Rais wa Singapore tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia 1980.
Ziara hii inaashiria hatua muhimu katika kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore.
Akiwa nchini Mheshimiwa Rais Tharman atapokelewa rasmi na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Ikulu Dar es Salaam na kuwa na mazungumzo rasmi kuhusu namna ya kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya biashara, uwekezaji, uchumi wa kidijitali, maendeleo ya bandari, elimu, mafunzo ya ujuzi, utalii na miundombinu.Ziara hiyo pia itajumuisha ushiriki katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji kati ya
Tanzania na Singapore pamoja na ziara Zanzibar kwa mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi.
Ziara hiyo inatarajiwa kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kiuchumi na kuimarisha uhusiano wa muda mrefu kati ya mataifa hayo mawili kwa manufaa ya wananchi wake.





Post a Comment