KASI YA MAENDELEO DAR ES SALAAM INACHANGIA ONGEZEKO LA MAHITAJI YA UMEME- MHE. KAPINGA

Na JUMANNE MAGAZI 

Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga  amesema ukuaji wa kasi wa maendeleo na uchumi katika Mkoa wa Dar es Salaam unachangia kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa ongezeko la mahitaji ya umeme.

Ameyasema hayo leo 18 Novemba, 2024  wakati wa ziara yake kwenye Kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi jijini Dar es Salaam iliyolenga  kukagua maendeleo ya maboresho ya miundombinu ya umeme katika kituo hicho ili  kukiongezea uwezo. 

Kituo  hicho kinachohudumia wakazi wa Gongo la Mboto, Mbagala, Kigamboni na Dege kinafungwa Transfoma yenye uwezo wa jumla ya 400 MVA  huku Transfoma za ukubwa wa 175 MVA zikiwa zimeshafungwa.

‘’ Lengo letu ni kuhakikisha Watazania hawakosi umeme kwenye kipindi chote cha maboresho kwani tunao umeme wa kutosha ili kukabiliana na kasi ya ukuaji wa maendeleo ya kiuchumi na Viwanda.’’ Amesema Mhe. Kapinga

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mha. Gissima Nyamo-Hanga amesema hatua zinazochukuliwa kuboresha hali hiyo ni pamoja na kuboresha njia ya kusafirisha umeme msongo wa kikovoti 220 kutoka Kimara-Ubungo-Mabibo  hadi Ilala na ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Mabibo ili kupunguza mzigo kwenye kituo cha Ilala sambamba na kuboresha njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa Kilovoti 220 kutoka Ubungo hadi Ununio na hivyo kunufaisha pia Zanzibar.

Mkoa wa Dar es Salaam unapata umeme kutoka vyanzo mbalimbali ikiwemo Gesi Asilia ambapo mahitaji ya umeme ni wastani wa Megawati 602 huku Mkoa wa Pwani mahitaji yakiwa  Megawati 136  na hivyo  kufanya ukanda wote wa Pwani na Dar es Salaam kuwa na mahitaji ya megawati 738.

 

Powered by Blogger.